Beginners Guide to TikTok for Search - Rachel Pearson - We are Tilt __ Bright...
The Standard: Enock Maregesi
1. ENOCK MAREGESI
MSHINDI WA PILI WA TUZO YA
KISWAHILI YA MABATI-CORNELL YA
FASIHI YA KIAFRIKA 2015
MWANDISHI WA KOLONIA SANTITA
MAHOJIANO
2. Ulianzaje kuandika?
Nilianza kuandika kwa kujijengea
utamaduni. Utamaduni wa kuandika.
Popote pale nilipoona kitu ambacho
nilidhani kilifaa kuandikwa mahali,
nilikiandika bila kusita au kuchelewa kwa
namna yoyote ile. Nilianza kwa kuandika
insha na kitu chochote kile kama vile
barua kwa rafiki yangu wa kike wa
kipindi kile, marafiki na kwa familia
yangu pia. Hicho ndicho kilichoniingiza
katika biashara hii ya uandishi wa vitabu.
3. Hadithi yangu ya kwanza kabisa
kuandika iliitwa Magaidi wa
Namba One – Namba One likiwa
jina la sehemu – hadithi fupi ya
kijasusi iliyohusu genge la
kijambazi, lililokuwa na maskani
yake mjini Dodoma. Magaidi wa
Namba One ilikuwa na urefu wa
kurasa 15. Niliiandika nikiwa na
umri wa miaka 15 au 16 hivi, katika
Shule ya Sekondari ya Bihawana ya
mkoani Dodoma.
4. Hadithi hii ilihusu kikundi cha
kigaidi kilichoitwa Namba One.
Kikundi hiki kilikuwa na makao yake
makuu nje ya Dodoma, katika pori
la Namba One, kama unaelekea
Iringa. Lilifanya shughuli zake ndani
na nje ya Dodoma hadi siku moja
mkubwa wake alipokamatwa; na
baadaye kupata adhabu ya kifungo
cha maisha jela kilichoambatana na
kazi ngumu, katika gereza lenye
ulinzi mkali la mkoani Shinyanga.
5. Baada ya hapo, viongozi wote wakubwa
wa kikundi hicho walikamatwa na
kukabidhiwa vifungo kulingana na
makosa waliyoyafanya.
6. Nini kilikusukuma kuwa mwandishi wa vitabu?
Nilihamasishwa na watu wengi na
matukio mengi kuwa mwandishi wa
vitabu: Ngugi wa Thiong’o, Ben Mtobwa,
Euphrase Kezilahabi, Penina Mlama,
Shafi Adam Shafi, sinema za mapigano
kama vile The Big Boss ya Bruce Lee na
Missing in Action ya Chuck Norris,
hadithi kutoka kwa wazee na watu
wengine wakubwa, na kadhalika.
7. Hata hivyo, hamasa kubwa zaidi
kushinda zote ilitoka kwa Shaaban
Robert – mzalendo wa kweli wa
Tanzania na kinara wa lugha ya
Kiswahili – ambaye vitabu vyake vilinipa
nguvu (na tumaini) kuandika riwaya
yangu ya kwanza ya Kolonia Santita,
ambayo awali iliitwa Salina Cruz.
8. Salina Cruz ni mji wa mwambao wa
kusini-magharibi mwa Meksiko,
katika jimbo la Oaxaca, kateli ya
Kolonia Santita ilipoanzishwa.
9. Nilipomaliza masomo yangu ya
sekondari mwaka 1992 nilianza kuandika
Kolonia Santita. Kipindi hicho nilikuwa
nikisubiri majibu ya mtihani wa taifa wa
kidato cha nne. Siku moja (nilipoanza
rasmi kuandika, miaka 23 iliyopita)
niliijiwa ghafla na ndoto ya mchana
nikiwa katika bustani ya nyumbani kwetu
Kijitonyama, Dar es Salaam. Vita kubwa
ya mawazo iliendelea kichwani mwangu
kwa muda mrefu bila kukoma, kuhusiana
na dhana fulani ambayo nilikuwa bado
sijaielewa sawasawa.
10. Ndoto hiyo ikawa msingi wa taaluma
yangu ya uandishi wa vitabu na msingi
wa utetezi wangu wa lugha ya Kiswahili.
Ikanikumbusha uzuri wa kipaji na uwezo
wa talanta nilivyopewa na Mungu na
jinsi gani nivitumie, na ikanikumbusha
jinsi gani nilivyoweza kuwa na uwezo
mkubwa kuburudisha na kuelimisha
watu kwa nguvu ya neno.
11. Ujasiri wa kujaribu au jeuri ya kufanya
kitu na kujiamini na tumaini, ulinipa
msingi wa kufikiri vyema na kuandika
kwenye karatasi dhana mbalimbali na
mawazo kadha wa kadha kutoka katika
dunia niliyoigundua. Nilikuwa na
uwezo, nilidhani, wa kuwa mojawapo
kati ya watoa burudani bora na
waandishi bora wa vitabu Tanzania.
12. Bustanini nilitamani sana kuchapisha
kitabu changu nje ya Tanzania na Afrika,
mathalani Uingereza au Marekani,
ambapo uchapishaji wa vitabu ni wa
kimataifa na wa daraja la kwanza.
Kichwa changu kilifikiria riwaya ambayo
ingesimulia mandhari ya miji zaidi ya
minne ulimwenguni kote, ambayo
baadaye ingekuwa ya kwanza kwa
mauzo hapa Afrika ya Mashariki na Kati.
14. Hadithi ya Kolonia Santita niliiandika kwa
miezi mitatu mfululizo hadi
nilipokamilisha rasimu ya kwanza kabisa
ya muswada wenyewe. (Nilikuwa na
umri wa miaka 20 nilipofanya hivyo). Kila
nilipodhani muswada umekamilika ili
niupeleke kwa wachapishaji, niligundua
bado ulihitaji marekebisho.
15. Mwaka 1999 hata hivyo nilidhani
umekamilika, na niliupeleka Popular
Publications Ltd (PPL) kwa ajili ya
mkataba wa uchapishaji wa vitabu.
Lakini PPL waliukataa muswada huo.
Waliukataa kutokana na ripoti iliyokuwa
na mchango mkubwa kwangu ya Hayati
Saifu D. Kiango, ambaye kipindi hicho
alikuwa mhariri mwandamizi wa Baraza
la Kiswahili la Tanzania (BAKITA).
16. Kiango alishauri katika ripoti yake
masahihisho mengi katika muswada
wangu, ambayo yote nilikubaliana nayo,
kabla sijaurudisha kwa wachapishaji
lakini nikashindwa kufanya hivyo.
Nilishindwa kuurudisha kwa
wachapishaji.
17. PPL walipoteza baadhi ya sura za
muswada wa Kolonia Santita (sura ya 7,
8 na 9) na sikufurahishwa na majibu
niliyopewa na Ndg. Mhando (nimesahau
majina yake mengine) kwamba
yeye/ofisi hawakujua hizo sura
zilipokwenda na kwamba yeye/ofisi
walipeleka muswada BAKITA ukiwa
umekamilika kabisa. Mhando alikuwa
mhariri mwandamizi wa PPL.
18. Kwa sababu hiyo niliuondoa
muswada wangu PPL na kuweka
nadhiri ya kusahihisha kila kosa
aliloliona Kiango na kushauri
nilisahihishe, na nadhiri ya
kuchapisha kitabu hicho mimi
mwenyewe nje ya Afrika kama
ningepata nafasi.
19. Mnamo mwaka 1992 hadi 1999 nilipata
nafasi ya kuandika miswada mingine
mitano. Miwili kati ya miswada hiyo
ilikuwa imekamilika. Mitatu ilikuwa
bado. Mitatu ni ya kipelelezi. Miwili ni ya
kimapenzi. Septemba 2004 nilihamia
London nchini Uingereza. Huko nilipata
nafasi nzuri zaidi ya kufanya utafiti
yakinifu, wa miswada yangu yote sita,
kwa kiwango nilichokitaka.
20. Katika maisha yangu yote
nilitamani sana kuwa mtetezi wa
lugha na utamaduni wa Kiswahili.
Nadhani tunahitaji wote kuwa
watetezi wa lugha hii na lugha
zingine za Kiafrika kwani hizi ndiyo
utambulisho wa bara letu.
21. Kutokana na hamu hiyo, mwaka
1995 niliweka nadhiri ya kupigania
lugha ya Kiswahili maisha yangu
yote yaliyobakia. Lakini nilijua hilo
lisingewezekana bila kwanza
kufanikisha elimu.
22. Mwaka 2010 nilijiunga na chuo cha
ubunifu wa kifasihi cha Manchester (The
Writers Bureau) nchini Uingereza, kwa
lengo la kutimiza ndoto zangu na kupata
taaluma ya uandishi wa vitabu. The
Writers Bureau walinipa moyo wa
kujiamini. Nilikuwa nikiishi shimoni,
gizani. Hata hivyo, baada ya kupitia
vitabu vichache vya kozi niliona nuru
upande wa pili wa tobwe.
23. Nilijua, kutokea kipindi hicho kwamba,
endapo ningesoma kwa bidii ningepata
uzoefu na utaalamu na mwongozo hasa
niliyoutaka. Nilitamani kuwa
mwandishi bora wa vitabu na
nilitamani kuwaelimisha watu na
kuwaburudisha pia. Nilitamani kuwa
mojawapo ya waandishi bora wa vitabu
na wauzaji bora wa vitabu nchini
Tanzania, na nje ya hapo.
24. Ulishindaje?
Habari ya Tuzo ya Kiswahili ya Mabati-Cornell
ya Fasihi ya Kiafrika niliipata kwa mshangao
mkubwa. Kwanza, niliipata kutoka kwa
Mkurugenzi wa CDEA (Culture for Development
East Africa) Ayeta Anne Wangusa mwezi wa
tatu 2015 ofisini kwake Dar es Salaam. Kisha
nikaandaa muswada wangu vizuri na kuutuma
kupitia tovuti ya tuzo kwa waamuzi wa tuzo,
kwa ajili ya mashindano.
25. Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya
Tuzo ya Kiswahili ya Mabati-Cornell ya
Fasihi ya Kiafrika Profesa Abdillatif
Abdalla aliponipigia simu kunijulisha
kwamba muswada wangu ulishinda
nafasi ya pili nilifurahi sana. Nilifurahi
sana kiasi kwamba nilijifungia chumbani
kwangu hotelini na kucheza muziki kwa
masaa matatu mfululizo, na nimekuwa
na furaha kuanzia kipindi hicho na
kuendelea.
26. Sababu kubwa ya muswada wangu
kushinda ni kujitahidi kwa kadiri ya
uwezo wangu WOTE. Ni uvumilivu,
uchapakazi na nidhamu.
27. Nini ushauri wako kwa waandishi chipukizi?
Ushauri wangu pekee ninaoweza
kutoa kwa waandishi chipukizi ni
elimu! Hutaweza kufikia malengo
yako kikamilifu bila msaada wa
wataalamu – Hata kama una kipaji
au ujuzi kiasi gani.
28. Ukiwa na kipaji nenda shule kurekebisha
kipaji chako, ukiwa na ujuzi nenda shule
kurekebisha ujuzi wako.